advanced Search
KAGUA
13969
Tarehe ya kuingizwa: 2012/04/07
Summary Maswali
hadi kufia leo, ni watu gani walio weza kusimama mbele ya shetani, na walitumia njia gani katika kupambana naye?
SWALI
shetani na jeshi lake la kijini tokea zamani wameamua kukabiliana na wacha Mungu na kupambana nao kupitia aina mbali mbali za mashambulizi, hufanya hivyo kwa ajili ya kuwalazimisha wacha Mungu kumkufuru Mola wao. Je hadi leo kuna watu wowote wale walioweza kusimama kidete na kupingana na mashetani hao, na kama jawabu itakuwa dio, basi ni njia gani walizozitumia watu hao katika kupambana na mashetani hao? Naomba jawabu muwafaka. Ahsanteni sana kwa juhudi zenu.
MUKHTASARI WA JAWABU

Kwa mtazamo wa Qur-ani ni kwamba: shetani hana uwezo wa kuwamiliki na kuwadhibiti wacha Mungu wenye ikhlasi na Mola wao.

Wacha Mungu wenye ikhlasi, ni wale walio ifikia daraja maalumu ya ucha Mungu, jambo ambalo huwa ndiyo ngao iwalindayo kutokana na shetani. Kupambana na shetani kunahitajia zana na silaha maalumu, na kupitia silaha hizo mja huwa ndiye mshindi atakayemtupa chini shetani ndani ya uwanja wa mieleka na kuibuka na medali ya ushindi. Baadhi ya silaha hizo za kupambana na shetani, ni kama ifuatavyo:

  1. Imani (itikadi madhubuti): Qur-ani takatifu imeihesabu imani kuwa ndio silaha msingi itakayomfanya shetani ashindwe kumdhibiti mja.
  2. Kutawakali (kumtegemea Mola): kumtegemea Mola ni silaha nyengine imuwezeshayo mja kumshinda adui yake (shetani), pamoja na jeshi lake.
  3. Kujilinda kupitia Mola Muweza: kumuweka Mola kuwa Ndiye ngao, ni njia muhimu ya kumshinda shetani.
  4. Kumtaja Mola (au kumkumbuka Mola kila wakati): kumkumbuka Mola wakati wote, ni jambo linalomfanya mja aepukana na wasi wasi utokanao na shetani, wasi wasi ambao huwa ndio njia kuu ya shetani.
  5. Kuwa na taqwa (ucha Mungu): ucha Mungu ni nguzo inayoyafungua macho ya moyo, macho ambayo humfanya mja auone vyema wasi wasi wa shetani na kuepukana nao.
JAWABU KWA UFAFANUZI

Kwa mtazamo wa Qur-ani ni kwamba: shetani huwa ni mtawala ndani ya nyoyo za wale wenye maradhi ndani ya nyoyo zao, lakini yeye (shetani) hana mamlaka yoyote yale katika kuwadhibiti wacha Mungu, na ukweli huu umethibitishwa na shetani mwenyewe, kama vile Qur-ani inavyo tuthibitishia hilo kwa kusema:

"قَالَ فَبِعِزَّتِكَ لَأُغْوِيَنَّهُمْ أَجْمَعِينَ ‏‏ إِلاَّ عِبَادَكَ مِنْهُمُ الْمُخْلَصِينَ"

Maana yake ni kwamba: (Akasema (shetani) nami ninaapa kwa Utukufu wako kwamba, mimi nitawapotosha wanaadamu wote, isipokuwa tu wale waja wako ambao ni miongoni mwa wacha Mungu (wenye ikhlasi).)[1]

Pia tunaweza kuufahamu ukweli huu kupitia Aya isemayo:

" إِنَّ عِبادي لَيْسَ لَكَ عَلَيْهِمْ سُلْطانٌ إِلاَّ مَنِ اتَّبَعَكَ مِنَ الْغاوينَ "

Maana yake ni kama ifuatavyo: (Kwa hakika waja wangu huna uwezo nao wa kuwamiliki na kuwadhibiti, ila wale watakaokufuata na kukutii miongoni mwa wale waliopotoka (hao ndio utakaowadhibiti).)[2]

Kwa jinsi ya maelezo ya Aya hizi ni kwamba: kundi pekee liwezalo kuepukana na uvamizi wa shetani, ni lile kundi la wacha Mungu (wenye ikhlasi), na ukweli huu umesemwa na shetani mwenyewe, na pia Mola Mtukufu ameutilia mkazo ukweli huo pale aliposema:

"إِنَّ عِبَادِي لَيْسَ لَكَ عَلَيْهِمْ سُلْطَانٌ"

Maana yake ni kwamba: (Kwa hakika wewe (shetani) huna mamlaka  wala uwezo wa kuwadhibiti waja wangu).

Njia za kukabiliana na shetani

Wenye ikhlasi ni wale walioifikia daraja maalamu miongoni mwa daraja za ucha Mungu, daraja ambayo huwa ndio ukuta na ngao imzuiayo shetani kupenya na kuwahujumu waja hao. Kukabiliana na shetani kunahitajia nyenzo na njia maalumu, nyenzo ambazo humuwezesha mja kupambana na shetani na hatimaye kuibuka na ushindi kutoka katika uwanja wa mieleka baina ya waja na mashetani. Sisi hapa tutatumia fursa hii katika kuelezea baadhi ya njia na nyenzo za kukabiliana na shetani kama ifuatavyo:

  1. Imani na itikadi madhubuti ni moja kati ya misingi mikuu iliyozingatiwa na Qur-ani ikiwa ni kama silaha madhubuti ya kupambana na shetani. Qur-ani ikizungumzia ukweli huu imesema:

‏"إِنَّهُ لَيْسَ لَهُ سُلْطَانٌ عَلَى الَّذِينَ آمَنُواْ وََ..."

Maana yake ni kwamba: (Kwa hakika shetani hana mamlaka wala nguvu za kuwadhibiti waumini…).[3]

  1. Njia na nyenzo nyengine ya kukabiliana na shetani na jeshi lake, ni kumtegemea Mola Mlezi. Mwenye Ezi Mungu kuhusiana na hili amesema:

" إِنَّهُ لَيْسَ لَهُ سُلْطَانٌ عَلَى الَّذِينَ ... وَعَلَى رَبِّهِمْ يَتَوَكَّلُونَ "

Maana yake ni kwamba (Kwa hakika yeye (shetani) hana mamlaka juu ya wale… ambao ni wenye kumtegemea Mola wao.)[4]

Kumuamini Mola pamoja na Aya zake ni ngome bora inayomfanya mja aepukane na utawala wa shetani, na kwa wale waliojikinga kupitia ngao ya imani huku wakimtegemea Mola wao katika kujilinda kwao na shetani, hao hawatotiwa mkononi na kutawaliwa na shetani. Kwani nguvu za utawala wa shetani huwa zinawadhibiti na kuwatawala wale tu waliokubaliana na utawala huo huku wakimshirikisha Mola wao. Na kuhusiana na jambo hili Qur-ani takatifu inasema:

"إِنَّمَا سُلْطَانُهُ عَلَى الَّذِينَ يَتَوَلَّوْنَهُ وَالَّذِينَ هُم بِهِ مُشْرِكُونَ"

Maana yake ni kwamba: (Kwa hakika mamlaka ya utawala wake (shetani) huwa juu ya wale wenye kumfanya yeye kuwa ndiye mtawala wao na wale wenye kumshirikisha Mola wao).[5]

3-    Kujilinda kumpitia Mola Mtakatifu: kujilinda tunakokumaanisha hapa, ni kutaka msaada kutoka kwa Mola Mtukufu. Kumuomba Mola msaada kunaweza kukawa kwa ajili ya kutaka kuepukana na moja kati ya aina mbili za shari, afu zote mbili kwa pamoja, aina ya kwanza ni kumuomba Yeye msaada kutokana na shari zinazotokana na hali halisi ya maumbile ya ulimwengu yanavyo kwenda, na ya pili ni kumuomba Yeye msaada kutokana na wasi wasi wa shetani pamoja na shari za walimwengu. Bila shaka ndani ya ulimwengu huu kuna aina mbali mbali za motokeo ya hatari, matokeo ambayo huwa ima yanatokana na nyenendo za walimwengu katika kuleta ufisadi ndani ya ulimwengu huu, au kwa wakati mwengine huwa yanatokana na maumbile ya dunia yalivyo. Na kwa upande wa pili pia huwa kuna maotokeo ya hatari na shari maalumu zinazosababishwa na nafsi za wanaadamu au majini. Mola Mtukufu akimtahadharisha Mjumbe wake (s.a.w.w) pamoja na kututahadharisha sisi kwa ujumla, amesema:

" وَ إِمَّا يَنْزَغَنَّكَ مِنَ الشَّيْطانِ نَزْغٌ فَاسْتَعِذْ بِاللَّهِ إِنَّهُ سَميعٌ عَليم‏"

Maana yake ni kwamba: (Na iwapo utapata aina fulani ya wasi wasi utokao kwa shetani, basi jilinde na Mola wako, kwani Yeye ni mwenye kusikia na ni mjuzi).[6]

Msingi wa imani ni wenye kumfanya mja amtegemee Mola wake katika kutafuta kheri na manufaa yake, na kule mja kuaza kazi au matendo na ibada zake za kila siku kwa jina la Mola wake, ni alama na dalili tosha zinazoonesha tegemeo lake kwa Mola wake, kwani kila mmoja wetu ni mwenye kuelewa kwamba: hakuna yeyote yule awezae kumnufaisha au kumdhuru mja, bila ya kupata idhini kutoka kwa Mola wake.

4- kumkumbuka Mola katika wakati wote: kuwa pamoja na Mola kila wakati, huwa kunamfanya mja awe na uoni wenye kumuepusha yeye na wasi wasi wa shetani, kwani kumkumbuka mola kila wakati ni ngao imara ya kumtenga mja na shetani.[7]

Imamu Saadiq (a.s) amesema: (shetani hana uwezo wa kumtia mtu wasi wasi, isipokuwa pale mja huyo atakapoghafilika na Mola wake).[8] Imau Ali (a.s) naye amesema:

"ذکرالله مطردة الشیطان."

Maana yake ni kwamba: (Kumkumbuka Mola (kumtaja Mola) ni jambo lenye kumkimbiza shetani).[9]

5- Ucha Mungu: kuifikia daraja ya ucha Mungu na kuilinda isitokomee, ni jambo lenye kumfungua mtu macho ya moyo wake, na iwapo moyo wa mtu fulani utakuwa macho, basi mtu huyo hato hujumiwa na wasi wasi wa shetana, Mola wetu anasema:

" إِنَّ الَّذينَ اتَّقَوْا إِذا مَسَّهُمْ طائِفٌ مِنَ الشَّيْطانِ تَذَكَّرُوا فَإِذا هُمْ مُبْصِرُون‏"

Maana yake ni kwamba: (Kwa hakika wale wacha Mungu pale wanapohujumiwa na wasi wasi wa shetani, huwa wanamkumbuka Mola pamoja na hatari ya siku ya malipo, na papo hapo hugutuka na kuuona uhakika wa mambo yalivyo).[10]

Neno (طائِفٌ) katika Aya iliyopita, lina maana ya kuzunguka, hii ina maana ya kwamba: wasi wasi wa shetani huwa unamzunguka mtu kutoka kila pembe kwa ajili ya kutaka kumghilibu, huku wasi wasi huu ukisubiri aina fulani ya udhaifu ili uweze kuitumia fursa hiyo kwa ajili ya kumpotosha mwanaadamu huyo.

Lakini iwapo mja atakuwa ana chumo na rasili mali ya taqwa (ucha Mungu), hapo shetani hatoweza kupata upenyo wa kumuingia na kumhujumu mja huyo.

Pia njia ya kupambana na shetani, ni kule mja kufanya jitihada za kukaa na watu wema huku yeye akichukua jitihada za kutenda mema na kutengana na waovu pamoja na maovu yao.

Natija ya utafiti

Kuwa na itikadi madhubuti, ni ngao bora kwa mja yenye kumuepusha yeye kutenda maovu. Vile vlie kumtafakari Mola pamoja na uwezo wake, kunaweza kumpa mtu natija ya kuikuza na kuipa nguvu nafsi yake kwa ajili ya kupambana na shetani. Pamoja na hayo, kuikuza imani na kumtegemea Mola pamoja na kumkumbuka Mola katika wakati wote, ni mambo muhimu ambayo hujenga nguvu madhubuti za kukabiliana na shetani, lakini pia mja asisahau kujilinda na kutaka msaada kutoka kwa Mola wake, pale anapokutana na mambo machafu, na bado sis tusisahau pia kuomba msaada kutoka kwa wanachuoni na mawalii wa Mola kwa ajili ya kujilinda na shetani pamoja na jeshi lake.

Tunamshukuru muulizaji wetu kwa swali lake hili muhimu, kwani yeye amekuwa ndiyo sababu ya kuandikwa kwa makala hii.

Ahsanteni sana, Mungu akubarikini pamoja nasi, aamin.

 


[1] Suratul-Israa, Aya ya 65.

[2] Suratu Hijri, Aya ya 42.

[3] Suratun-Nahlli, Aya ya 99.

[4] Rejea rejeo lililopita.

[5] Rejea rejeo lililopita, Aya ya 100.

[6] Suratul-Aa’raafi, Aya ya 200, na Fussilat, Aya ya 36.

[7] Rejea Auratul-Aa’raafi, Aya ya 201.

[8] Mustadrikul-Wasaaili, cha Muhaddithu Nuuriy juz/1, uk/178, chapa ya Aalul-Bait, Qum, mwaka 1408 Hijiria. Bihaarul-Anwaaru, cha Muhammad Baaqir Majlisiy, juz/72, uk/124, chapa ya Al-Wafaa, Beirut, mwaka 1404 Hijiria.

[9] Ghurarul-Hikami-wa Durarul-Kalimi, cha Abdul-Waahid Amadiy Tamiimiy, uk/188, chapa ya Maktabul-Ii’laamil-Islaamiy, Qum, mwaka 1366 Shamsia.

[10] Suratul-Aa’raafi, Aya ya 201.

 

TARJAMA YA JAWABU KATIKA LUGHA NYENGINE
MAONI
Idadi ya maoni 0
Tafadhali ingiza thamani
mfano : Yourname@YourDomane.ext
Tafadhali ingiza thamani
<< Niburute.
Tafadhali ingiza kiasi sahihi ya usalama Kanuni

MPANGILIO WA KIMAUDHUI

MASWALI KIHOLELA

YALIYOSOMWA ZAIDI